Jacqueline Patrick ‘Jack’.
MODO
mwenye mvuto Bongo Jacqueline Patrick ‘Jack’, ambaye yuko mahabusu ya
Gereza la Qincheng nchini China kwa madai ya kunaswa na madawa ya
kulevya nchini humo, anazidi kuteseka, safari hii akidaiwa kukabiliwa na
tatizo kubwa la kiafya.
Kwa mujibu wa chanzo chetu, Jack anasumbuliwa na ugonjwa wa kukosa
hamu ya kula, hali iliyomfanya apoteze uzito wa kilo kumi huku
akikabiliwa na tatizo lingine la kupungua kwa kasi ya mapigo ya moyo.
KAMA HALI ITAENDELEA
Chanzo
kimesema kuwa endapo hali ya kuzorota kwa afya hiyo kutaendelea, Jack
anaweza kujikuta katika tatizo kubwa zaidi ambalo linaweza kusumbua
kwenye mwenendo mzima wa kesi yake.
“Kusema
kweli kuhusu maisha ya mahabusu si mabaya sana kwake, hateswi kwa
kupigwa wala hanyimwi chakula, ila hana uhuru binafsi, ni kama
amefichwa, naamini matatizo hayo ya kiafya yanatokana na uzito wa kesi
yake,” kilisema chanzo hicho.
MLOLONGO WA MAMBO
Habari
zaidi zinadai kwamba kesi ya msingi ya staa huyo kudaiwa kukutwa na
madawa ya kulevya itaanza kusikilizwa rasmi Septemba, mwaka huu baada ya
mwanasheria wake kukamilisha taratibu zote.
“Ile kesi yake sasa ni
Septemba mwaka huu. Si unajua hajawahi kupandishwa kizimbani kuulizwa
kama ni kweli alikamatwa na unga au la!” kilisema chanzo hicho.
Jack Patrick akiwa amefunikwa uso baada ya kukutwa na pipi za heroin tumboni nchini China.
WAKILI WAKE ANATOKA HONG KONG
Taarifa
zaidi zinasema kuwa wakili wa mrembo huyo anatoka jijini Hong Kong
nchini humo ambako ndiko kwenye wanasheria wazuri kwa kiwango cha kesi
yake ya unga.
KUMWONA NI KWA AHADI
Ikazidi
kudaiwa kwamba kuna Mtanzania mmoja tu ambaye amekuwa na fursa ya
kumuona modo huyo na kabla ya kwenda lazima aombe na kupewa
‘apointimenti’ maalum.
WALIOMTUMA WAMPIGA CHENGA, WALA ‘BATA’
Tofauti
na kwa Video Queen wa Bongo, Agnes Gerald ‘Masogange’ ambaye naye
aliwahi kupata msala mkubwa kama huo nchini Afrika Kusini, Julai, mwaka
jana ambapo ‘mabosi’ wake walikuwa mstari wa mbele kumhangaikia, Jack
anasota mwenyewe.
Habari
zinasema kuwa hakuna cheni yoyote kutoka kwa watu ambao wanatafsiriwa
kuwa ni waliomtuma kwani wanaosumbuka ni watu wake wa karibu, wakiwemo
ndugu zake.
Juzi, Risasi Mchanganyiko lilizungumza na mtu wa karibu sana na
mtuhumiwa huyo ambapo alikiri Jack kuwa na hali ngumu katika kesi yake
hiyo huku akisema kwamba watu wanaodaiwa ndiyo mabosi wake wanakula
‘bata’ tu jijini Dar es Salaam.
“Unajua tatizo la biashara ya unga ni hapo tu! Wewe unayebeba
ukinaswa ni juu yako, waliokutuma wao wanachofanya ni kuthibitisha tu
kuwa ni kweli umekamatwa maana wapo wanaodaiwa wamekamatwa kumbe si
kweli, wanaingia mitini na mzigo,” alisema mtu huyo.
SABABU ZA MOYO KUSHINDWA KUSUKUMA DAMU
Juzi,
gazeti hili lilimtafuta daktari mmoja wa Hospitali ya Taifa Muhimbili
(jina lipo) na kumuuliza tatizo la moyo kushindwa kusukuma damu ambapo
alisema:
“Moyo kushindwa kusukuma damu kwa mwendo wa kawaida husababishwa na
shinikizo la damu lisilodhibitiwa, mgonjwa kushindwa kudumisha udhibiti
wa maji mwilini, chakula au dawa.
“Sababu nyingine ni upungufu wa damu na utoaji wa kiwango cha juu cha
homoni za koromeo ambazo zinaleta maumivu ya ziada kwenye misuli ya
moyo, utumiaji mwingi wa vimiminika au ulaji wa chumvi uliopitiliza na
utumiaji wa dawa ambazo husababisha uwekaji wa maji mwilini kama vile
Hiazolidinedione.”
KUHUSU KUKOSA HAMU YA KULA
Kwa
mujibu wa daktari huyo, tatizo hilo humkumba mtu anapokuwa katika
msongo mkubwa wa mawazo kutokana na jambo zito linalomkabili, ambalo
halina mlango wa kutokea.
TUKUMBUKE
Mrembo
huyo alikamatwa Desemba 19, mwaka jana katika Uwanja wa Ndege wa Macau,
China akitokea Bangkok, Thailand akiwa na kete 57 (kilo 1.1) za heroin
tumboni zikiwa na thamani ya jumla ya zaidi ya shilingi milioni 300.
Awali ilidaiwa kuwa kesi yake ingeanza kusikilizwa mwaka 2016 baada
ya yeye kujifunza Kireno (lugha inayotumika Macau) kwa miaka miwili.